Mwamuzi wa mchezo wa ligi kuu Tanzania Bara kati ya watani wa
jadi, Simba na Yanga, atafahamika uwanjani wakati wa mchezo huo,
kutokana na Shirikisho la Soka nchini (TFF) kuamua kuficha jina lake.
Afisa Habari wa shirikisho hilo, Alfred Lucas amesema wameamua kuficha
jina la mwamuzi huyo ili kupunguza uwezekano wa hujuma au hisia za
mwamuzi kununuliwa au kusumbuliwa na ama timu mojawapo au timu zote
mbili.
Lucas amesema TFF imeamua kujiwekea utaratibu huo ili kuepusha uwezekano
wa kutokea kwa vurugu kama zilizotokea katika mchezo uliopita, na sasa
timu zote mbili zimekwishataarifiwa kuwa mwamuzi wa mchezo huo
atafahamika siku ya mchezo wakati wa kikao cha maandalizi ya mechi.
(Pre-match meeting)
Kwa upande wa vilabu vyote Simba na Yanga, zimeonekana kukubaliana na uamuzi huo, ambapo kwa niaba ya Yanga, Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Salum Mkemi amesema wao wako tayari kwa mwamuzi yeyote hata awe anatoka Simba, ilimradi afuate sheria zote za soka.