banner

April 17, 2024

MBAPPE APIGA MBILI..PSG YAWANYAMAZISHA BARCELONA NYUMBANI 4-1

MBAPPE APIGA MBILI..PSG YAWANYAMAZISHA BARCELONA NYUMBANI 4-1


TIMU ya Paris Saint-Germain ya Ufaransa imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya wenyeji, FC Barcelona usiku wa kuamkia leo Uwanja wa Olímpic Lluís Companys Jijini Barcelona nchini Hispania.
Mabao ya Paris Saint-Germain yamefungwa na viungo, Mfaransa mwenye asili ya Mali, Masour Ousmane Dembélé dakika ya 40, Mreno Vítor Machado Ferreira ‘Vitinha’ dakika ya 54 na mshambuliaji Mfaransa mwenye asili ya Cameroon, Kylian Mbappe mawili dakika ya 61 kwa penalti na 89.
Bao pekee la Barcelona lilifungwa na mshambuliaji Mbrazil, Raphael Dias Belloli ‘Raphinha’ dakika ya 12 katika mchezo ambao wenyeji hao walimaliza pungufu kufuatia beki wake Ronald Araujo kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 29.
Refa Mromania, Istvan Kovacs pia aliwatoa kwa kadi nyekundu, Kocha wa Barcelona, Xavi na Kocha wake wa makipa, Jose Ramon De la Fuente kwa matokeo hayo PSG wanatinga Nusu Fainali kwa ushindi wa jumla wa 6-4 kufuatia kufungwa 3-2 kwenye mchezo wa kwanza Aprili 10 Uwanja wa Parc des Princes Jijini Paris.
Ikawa siku mbaya zaidi kwa Waspaniola baada ya Atlético de Madrid nayo kutolewa kufuatia kufungwa na wenyeji, Borussia Dortmund mabao 4-2 Uwanja wa Signal Iduna Park Jijini Dortmund nchini Ujerumani.
Borussia Dortmund wanakwenda Nusu Fainali kwa ushindi wa jumla wa 5-4 kufuatia kufungwa 2-1 kwenye mchezo wa kwanza Aprili 10 Uwanja wa Cívitas Metropolitano Jijini Madrid na sasa watakutana na PSG.


source http://www.binzubeiry.co.tz/2024/04/mbappe-apiga-mbilipsg-yawanyamazisha.html

Post a Comment

Whatsapp Button works on Mobile Device only

Start typing and press Enter to search